Monday, May 13, 2013

MAPOKEZI YA DK. KAFUMU BAADA YA KUREJESHEWA UBUNGE YALIVYOTIKISA IGUNGA


Mbunge wa Igunda, Dk. Peter Dalally Kafumu akiwasalimia wananchi katika mkutano wa mapokezi yake uliofanyika jioni hii kwenye Uwanja wa Sokoine mjini Igunga mkoani Tabora. Kuliani Katibu wa NEN, Itikadi na Uenezi CCM, Nape Nnauye.
*************************
NA BASHIR NKOROMO,IGUNGA
WAKATI mapokezi ya Mbunge wa Igunga Dk. Dalally Peter Kafumu yamesababisha baadhi ya shughuli kusimama, kwa hoi hoi, nderemo na 
vifijo, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimeahidi kuongeza kasi ya utekelezaji wa ahadi ilizotoa katika jimbo hilo.

Akizungumza kwenye mkutano wa mapokezi ya Dk. Kafumu uliofanyika kwenye Uwanja wa Sokoine mjini hapa, Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema CCM lazima itazitekeleza ahadi zote zilizotolewa na mbunge huyo kupitia ilani ya Chama wakapi akigombea katika uchaguzi mdogo uliofanyika 2011 jimboni humo.

"Baada ya mahakama kumrejeshea Ubunge mbunge wetu, CCM inaahidi kwamba ahadi zote alizotoa mbunge wenu zitatekelezwa kabla ya mwaka 2015. Na kwa kuwa Chadema walipunguza kasi kwa kusimamisha mbunge wenu baada ya kumpeleka mahakamani, CCM itaisimamia serikali ili kuhakikisha inaongeza kasi ya utekelezaji wa ahadi hizo kufidia pale utekelezaji ulipokuwa umepungua kasi", alisema Nape.

Alisema, licha ya Dk. Kafumu kusimamishwa na mahakama, CCM iliendelea kutekeleza ilani katika jimbo la Igunga, kwa sababu ni wajibu wake kutokana na kwamba CCM ndicho chama chenye ilani inayotelekezwa kutokana na kuvishinda vyama vyote katika uchaguzi mkuu uliopita.

Nape alisema, moja ya miradi ambayo Dk. Kafumu na CCM waliahidi  ni ujenzi wa daraja la mto Mbutu ambalo, alisema, sasa ujenzi wake unaendelea na yapo matumaini ya kukamilika kama ilivyopangwa.

Alisema, ahadi zingine ni kuhusu umeme, Barabara na afya ambavyo ni miongoni mwa mambo ambayo yapo katika ilani ya CCM, ambayo lazima CCM iyape kipaumbele kuhakikisha yanakamilika kuondoa au kupunguza kero za wana-Igunga.

Nape aliwataka wananachi wa Igunga kumpokea mbunge wao kwa mikono miwili na kumpa ushirikiano katika kutekeleza ahadi zake kwa sababu ni Mbunge ambaye wamepewa na Mungu wao na ndiyo sababu ameweza kurejeshwa na Mahakama licha ya juhudi za Chadema kujaribu kumkwamisha asiwatumikie.

"Hukumu ya kwanza tulishangaa, lakini kwa sababu tuliheshimu sheria kukatulia na kukata rufani. Mungu amekaa kati yenu wana Igunga amewarejeshea Dk. Kafumu", alisema Nape.

Akizungumzia hali ya kisiasa nchini, Nape aliwataka wanaigunga na Watanzania kwa jumla sasa kuwa makini na vyama vya siasa vilivyopo hapa nchini akidai baadhi vimegeuka kuwa vyama vya vurugu na vya kigaidi badala ya kuwa vya siasa kama ilivyokusufdiwa.

Nape aliwataka wananchi wa Igunga kuwatenga wanaoshabikia chama chochote kinachoonekana kuwa cha fujo na kuwa na mipango ya kigaidi.

Akizungumza kwenye mkutano huo, Dk. Kafumu alisema, amefarijika sana kurejeshewa ubunge, akisema anatambua kuwa yeye ndiye chaguo la ubunge kwa wana Igunga kwa kuwa wanamtumainia katika kushirikiana nao kwenye katika kuliendeleza jimbo lao na Tanzania kwa jumla.

Dk. Kafumu aliahidi kuendelea na utekelezaji wa ahadi zake alizowapa wananchi wa jimbo hilo, ikiwemo ujenzi wa dalaja katika mto Mbutu ambalo alisema kutokuwepo kwa daraja hilo kumekuwa moja ya voikwazo vya maendeleo jimboni.

"Alipokuwa nazungumza hapa (Nape) nimetamani kulia kama mtoto wa Mkulima (Waziri Mkuu Mizengo Pinda), kutokana na hisia zilizoniingia kutokana na maneno aliyosema. kwa hiyo sina mengi ya kusema zaidi ya kuwashukuru kwa kunitia moyo nilipokuwa sipo kama mbunge wenu, maana nimekuta baadhi ya ahadi zaungu zimeendelea kutekelezwa", alisema Dk. Kafumu.

"Napenda niwahakikishieni kwamba nitatekeleza ahadi zangu zote na sina shaka nitafanikiwa akwa kuwa mmenipa moyo mkubwa kwa mapokezi mliyonipa na hivyo naamini mtashirikiana nami kwa nguvu zaidi kutekeleza ahadi hizo", alisema.

Mapokezi ya Dk. Kafumu ambaye aliwasili saa nane alasirin akitokea Dodona na Nape, yalianzia kiasi cha kilometa tano nje ya mji ambapo ulienda kwa kusindikizwa na pikipiki zaidi ya 200 na bajaji zaidi ya 60 huku wengine wakitembea kwa miguu kwa shamrashamra hadi Ofisi ya CCM ya Wilaya ya Igumnga.

Kabla ya ubunge wake kutenguliwa na Mahkama baada ya Chadema kwenda mahakamani, baada ya kushinda katika uchaguzi mdogo uliofanyika mwaka 2011, kufuatia aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Rostam Aziz kujiuzulu.


 Wananchi wakimbeba Mbunge wa Igunga mkoani Tabora, Dk. Dalally Peter Kafumu kumpeleka jukwaani, wakati wa mkutano wa mapokezi yake, jimboni humo uliofanyika leo kwenye uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine mjini Igunga. Dk. Kafumu amerejeshewe ubunge na mahakama kuu baada ya kukata rufani kufuatia awali kuvuliwa pia na mahakama baada ya Chadema kwenda mahakamani aliposhinda katika uchaguzi mdogo wa jimbo hilo uliofanyika mwaka juzi

No comments:

Post a Comment