Monday, July 3, 2017

BAADHI YA WAKURUGENZI WA MANISPAA MBALIMBALI WASHIRIKI UZINDUZI WAKALA WA BARABARA MIJINI NA VIJIJINI (TARURA) MJINI DODOMA.

Mkurugenzi wa Manispaa ya Ubungo Jijini Dar es salaam Ndg John Lipesi Kayombo ameungana na wakurugenzi wengini nchini kuhudhuria Mkutano wa Uzinduzi wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini uliofanyika Kwenye Ukumbi wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere uliopo katika Chuo Cha Mipango Mjini Dodoma Leo Julai 2, 2017.
Mkurugenzi Kayombo ameshiriki Mkutano huo uliofunguliwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Kassim M. Majaliwa (MB) wenye dhamira ya kuleta mageuzi makubwa katika sekta ya Barabara nchini kutokana na kuanzishwa kwa wakala wa barabara Mijini na Vijijini.
Uanzishwaji wa Wakala wa Barabara nchini ni utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya Mwaka 2015 iliyopo katika ukurasa wa 54 inayoielekeza serikali kuanzisha Wakala/Taasisi itakayosimamia kazi za ujenzi na matengenezo ya barabara za Halmashauri, Miji, na Majiji ambazo zipo chini ya TAMISEMI ifikapo mwaka 2020.
Katika Mkutano huo zimeelezwa changamoto mbalimbali zinazozikabili mamlaka za serikali za Mitaa katika ujenzi, ukarabati na matengenezo ya miundombinu ya Barabara ambazo ni pamoja na Miradi kutekelezwa kwa viwango duni, Ucheleweshaji wa utekelezaji wa miradi kutokana na mipango isiyoridhisha, Kandarasi kutolewa bila kuzingatia vigezo, uwezo na sifa.
Changamoto zingine ni pamoja na kutokuwepo kwa viwango vinavyoshabihiana vya ubora wa barabara Kati ya Halmashauri Moja na nyingine, Fedha zilizopangwa kutekeleza miradi ya barabara kutotumika kutokana na urasimu wa viongozi wa Halmashauti, Rushwa iliyokithiri katika utoaji wa zabuni, Mgongano wa maslahi na usimamizi hafifu wa mikataba ya ujenzi.
Wakala huu utasaidia kuimarisha mtandao wa barabara za vijijini na hivyo kuwawesesha wananchi wengi zaidi kusafiri na kusafirisha bidhaa za mashambani kwa urahisi.
Katika Mkutano huo Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Majaliwa K. Majaliwa akizungumza kabla ya kuzindua Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini alieleza manufaa yatakayopatikana kutokana na kuwa na Barabara za Vijijini na Mijini kuwa ni pamoja na kuongeza chachu ya uzalishaji Mali mashambani kutokana na urahisi wa kufikisha mazao sokoni, Kushusha bei ya vyakula mijini kutokana na gharama za kusafirisha mazao kutoka mashambani kupungua.
Mengine ni kuboresha na kubadili hali za kimaisha na kiuchumi kwa wananchi, kufanya maeneo mengi zaidi ya nchi kufikika kwa urahisi na hivyo kuboresha utoaji wa huduma za kijamii na Kutoa ajira kwa vijana katika maeneo ambayo ujenzi au ukarabati wa miundombinu utakapokuwa unafanyika.
Katika Mkutano huo Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo, imewakilishwa na Mkurugenzi Kayombo ambaye ameambatana na Kaimu Mkuu wa Idara ya Ujenzi na Zimamoto Manispaa ya Ubungo Ndg Goodluck Mbanga.

No comments:

Post a Comment